
Leo jioni nilikula futari pale New Zahir Restaurant. Mahala pale wanakuja watu wa kada aina mbalimbali. Leo ilianzishwa mada ilikotea haijulikani,ilihusu waraka unaosemwa unaoandaliwa na Waislamu. Kila mmoja alisema lake, na mpaka naondoka pale New Zahir sikupata kujua uhakika wa chanzo cha habari ile. Baadae usiku huu nimesikia ikikanushwa na BAKWATA kuwa haihusiki na waraka huo.
Mahali pale, New Zahir Restaurant iliyopo mtaa wa Msikiti katikati ya jiji pana historia isiyojulikana na wengi,nilipata kuandika juu ya jambo hilo;
Kwamba Che Guevara aliwahi kutembelea mara kadhaa mgahawa huo wa ' Zahir Restaurant' kama ulivyojulikana wakati huo. Inasemekana Che Guevara aliingia Dar April 1965, alikutana na Nyerere na kupata baraka zake kuhusiana na ajenda yake ya kwenda Congo kuwasaidia wapiganaji wa Congo katika harakati za kuikomboa nchi yao. Che aliingia Mashariki ya Congo akiwa na kikosi cha askari 100; Hawa ni Wa-Cuba weusi waliopata mafunzo ya kijeshi Havana bila kuelewa kuwa walikuwa wanakwenda Congo. Uwepo wa Che Guevara jijini Dar April 1965 haukufahamika na wengi. Hata CIA hawakuelewa hilo. Hadi mwaka 1990 CIA waliamini kuwa Che Guevara aliingia Congo akitokea Congo Brazaville. Kwamba Che Guevara alikuwa Dar kwa juma moja na zaidi unadhihirisha ukweli wa simulizi kuwa Che Guevara alitembelea mgahawa wa Zahir ( Sasa New Zahir Restaurant) mtaa wa Msikiti na kuwa na mazoea ya kunywa chai na kula chakula mahala hapo. New Africa Hotel kulikuwa na mgahawa maarufu kule juu kabisa, lakini pale pangemfanya aonekane kirahisi hata na mawakala wa CIA. Che Guevara anamweleze Laurent Kabila ( Baba yake Joseph Kabila) kama mtu ambaye hakuwa makini katika kuendesha harakati za mapambano. Che anaandika kuwa Kabila alipenda sana pombe, hakuonekana kwenye uwanja wa mapambano, mara nyingi alituma ujumbe wa mdomo au maandishi kutoa maelekezo. Che alikwenda na kikosi chake Mashariki ya Kongo bila ya mwenyeji wake, Laurent Kabila. Laurent Kabila alikuwa na miaka 26 tu wakati huo. Kuhusu umri wa Kabila Che Gueavara anandika hivi; " Kabila is young, and it is possible that he will change. But I have very great doubts about his ability to overcome his defects in the environment in which he operates".