
Wanakijiji Wenzangu,
KWA mara nyingine tena, natuma salamu zangu hizi za kuuaga mwaka na kuukaribisha mwaka mpya wa 2010 nikiwa hapa Bagamoyo. Tofauti na mwaka unaomalizika, salamu zangu za Mwaka Mpya wa 2010 nazituma katika hali ya huzuni. Watanzania, katika siku hii ya mwisho ya mwaka, tumeondokewa na mtu muhimu sana katika historia yetu, Mzee Rashid Mfaume Kawawa. Atabaki kuwa kiongozi wa kupigiwa mfano, aliishi kama alivyohubiri. Historia ya nchi haitaandikwa ikakamilika bila kutajwa kwa mchango wa Mzee Kawawa. Vivyo hivyo, historia ya TANU na CCM haitaandikwa na kukamilika bila kutajwa kwa mchango wa Mzee Kawawa. Hata historia ya filamu na mpira wa miguu katika nchi hii haitaandikwa na kukamilika bila kutajwa kwa mchango wa Mzee Kawawa. Atakumbukwa daima.
Vinginevyo, mwaka unaoisha umekuwa wa matukio mengi ya kisiasa, kiuchumi na kijamii.Kijiji chetu hiki kimebaki kuwa chachu ya mijadala yenye kulenga kwenye kulinda maslahi mapana ya nchi yetu.
Mijadala mingi humu kijijini imekuwa yenye siha. Kwa baadhi yetu imekuwa ni darasa tosha la kujichotea maarifa mbalimbali. Na tuendelee kukifanya kijiji hiki kuwa chachu ya mijadala hata mwaka ujao wa 2010.
Nawatakia Heri Na Fanaka Kwa Mwaka wa 2010.
Maggid,
Bagamoyo. ( Pichani ni Bagamoyo jioni hii)














































.jpg)



