
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon akishiriki kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, kilichokuwa kikijadili tishio la Mtandao wa Uhalifu wa Kimataifa kwa usalama, amani na maendeleo ya Mataifa. ( Picha kwa hisani ya Umoja Wa Mataifa)
Na Mwandishi Maalum New York-Mtandao wa uhalifu wa kimataifa ambao umeelezwa kwamba sasa ni tishio lililodhahiri kwa maendeleo na usalama wa dunia. Unajijenga kwa kasi kubwa katika maeneo mbalimbali duniani ikiwa ni pamoja na meneo ya Afrika ya Magharibi, Kati na Mashariki.
Na kwa sababu ya tishio hilo, nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa zimetakiwa kuongeza kasi ya ushirikiano kwa kubadilishana taarifa mbalimbali zikiwamo za kitelejesia, kuongeza ulinzi mipakani, pamoja na kuimarisha utawala wa sheria na kupiga vita rushwa.
Bw. Antonio Maria Costa, Mkurugenzi Mtendaji Katika Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayohusika na madawa na uhalifu (UNODC) , ameonya kuwa mtandao wa uhalifu wa kimataifa unaohusisha biashara ya dawa za kulevya, silaha na ugaidi na utekaji nyara ina uwezo mkubwa wa kifedha na matumizi ya teknolojia za kisasa za mawasiliano kiasi kwamba si rahisi kwa nchi moja moja kukabiliana nao.
Alikuwa akiwasilisha taarifa ya ofisi yake mbele ya Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa, kuhusu mwenendo wa mtandao wa uhalifu wa kimataifa na tishio lake dhidi ya maendeleo, usalama na ustawi wa mataifa.
Akasema njia nyingine ya kudhibiti mitandao hiyo ya uhalifu wa kimataifa ni kupunguza nguvu zao za kifedha kwa kumata na kutaifa mali zao na kuziba mianya ya rushwa na fedha chafu, pamoja na kuzisaidia nchi za Afrika kuimarisha vyombo vyao ya sheria na kujikwamua na umaskini.
Katika kikao hicho ambacho pia kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, Mkurugenzi Mtendaji huyo ameeleza kwamba, kwa kutumia uwezo wao wa kifedha, wahalifu hao wa kimataifa wameweza kujipenyeza na kuweka mitandao yao hususani katika nchi maskini za Afrika , zenye migororo, zisizokuwa na utawala madhubuti unaozingatia sheria na zenye kukumbatia rushwa.
Akasema kuwa wauzaji wakubwa wa dawa za kulevya kwa kutumia faida kubwa wanayopata kupitia biashara hiyo, huangalia wapi penye udhaifu na kujipenyeza kwa kutoa rushwa, kuwatumia vijana wasio kuwa na ajira kuleta vurugu na machafuko katika nchi zao na hata kuzipindua serikali halali.
Akionyesha uwezo mkubwa wa kifedha wa mtandao wa biashara ya dawa za kulevya, Bw. Antonio Mario Cost anasema .
“ Bajeti ya matumizi ya kawaida ya ofisi yangu ni asilimia moja ya bajeti ya Umoja wa Mataifa, ambayo nayo ni chini ya asilimia moja ya faida wanayoipata wafanyabiashara wa kimataifa wa dawa za kulevya ambayo ni Dola 320 bilioni kwa mwaka”.
Akatoa mfano mwingine kwa kusema “Mstari mmoja wa mnuso wa Kokeini anaonusa mtumiaji wa kule Ulaya faida yake inanunua risasi 100 za AK-47 kule Afrika Magharibi. Sasa zidisha mara tani 850 za kokeini kwa mwaka utaona ni kama vile kumshindanisha Daudi na Goliath”
Akichangia majadiliano hayo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, amesema Jumuia ya Kimataifa kupitia Baraza Kuu la Usalama inatakiwa kujipanga upya kwa kubuni mbinu na mikakati ya kukabiliana na tishio hilo.
Akasisitiza Umoja wa Mataifa hauwezi kufumba macho na kujifanya kama vile haioni tishio la uhalifu wa kimataifa dhidi ya usalama na maendeleo.
“Hatuwezi kuzima moto kwa kutumia moto, wahalifu hawa wana mbinu nyingi na za kisasa ambazo hata hatuwezi kushindana nao kama kila nchi itapigana vita hii kivyake vyake. Lazima tukusanye nguvu zetu kama jumuia na tukidhamiria tunaweza” akasisitiza Ban Ki Moon.
Akasisitiza kuwa mataifa hayana njia mbadala zaidi ya kujijengea mazingira ya kuaminiana na kushirikiana kwa sababu kila nchi inaathirika au itaathirika na janga hili.
Mwisho mwa mkutano huo,wajumbe 15 wa Baraza Kuu la Usalama walikubaliana kwamba lazima sasa jumuia ya kimataifa iwajibike kwa pamoja katika kukabiliana na tatizo hilo.