
Ndugu Mjengwa,
Samahani kuchukua muda wa kutoa ufafanuzi wa kipengere kidogo katika habari yako au makala juu ya demokrasia. Ninakuomba uisome vizuri historia ya Uganda na baada ya hapo toa tathimini ya viongozi waliotangulia. Kwa kifupi, Waingereza waliacha uhuru wa Uganda kwa kabila moja tu nalo ni 'Baganda' (sawa kwa Z'bwe yaani chini ya Smith) na mfalme wao ndio aliyekuwa rais. Hivyo basi, Obote aliteuliwa na mfalme kuwa waziri mkuu. Kama ilivyokuwa kwa Tanganyika na Zimbabwe, mawaziri wakuu yaani Nyerere, na Mugabe waliondoa mfumo wa waziri mkuu kama mtendeji mkuu wa serikari na badala yake 'ceremonial president' ndio akachukua rungu. Na hili liko wazi, Uganda kama nchi haikuwa na mfumo wa kifalme ispokuwa kabila moja tu yaani Wa-baganda. Ikiwa Obote alilewa madaraka basi nitashawishika pia kuwa Nyerere na Mugabe nao walilewa madaraka (nafahamu suala la Mugabe ni exception). Ikiwa ndivyo basi wengi walilewa madaraka. La msingi ni kwamba ni katika utawala wa Obote (awamu ya kwanza) juhudi za kujenga misingi ya utaifa zilifanyika yaani kuondoa dhana kwamba Uganda si 'baganda' tu na makabila mengine ni kama vivuli. Ni katika kipindi cha Obote ndipo unapoweza kuona maendeleo yote ya Uganda ya leo, yaani ujenzi wa hospitali kuu ya Mulago, chuo cka Makerere, barabara za lami toka Malaba hadi Gulu, mbarara, na bandari ndipo ulipofanyika. Kumbuka misaada kutoka kwa wafadhili hadi 1985 ilikuwa ni $6 bilioni tu. Je unataka kumlinganisha Obote na Musevelini ambaye aliharibu barabara kwa kupitisha magari ya kivita, na leo hii kuzikarabati barabara alizoharibu ndio tuite maendeleo? Je zaidi ya taasisi alizoacha Obote nini zaidi kilichoongezeka? Kumbuka kutoka 1985 hadi leo Uganda imepokea misaada ya kiasi cha $22 billion kutoka nje na bado hakuna kinachoonekana. Katika kutimiza miaka 23 ya NRM mwaka 2009, chama hicho kiorodhesha mafanikio nane (8) tu! Je ni kweli ndani ya miaka 23 ni hayo tu! Vurugu zote zinazotokea Uganda ni kutokana na kwamba misingi ya utaifa aliyotaka kuijenga Obote haikufanikiwa au ilivurugwa na kabila moja. Kumbuka palikuwa na shule nzuri za serikali kipindi cha Obote ambazo hazikuwa Kampala tu, bali Lango, Arua, Soroti, hadi Jinja. Leo hii chini ya Museverini elimu nzuri ipo Kampala tu. Na ndio maana vijana wetu toka Tanzania wanaishia katika shule za Kampala na vitongoji vyake. Mfano ni kwamba katika matokeo ya kidato cha sita ya kitaifa, wanafunzi waliofanya mitihani na kupata alama 3A's (A,A,A), 90 walitoka kwenye wilaya tatu za Kampala na labda 6 sehemu nyingine za nchi. Ukikutana na kizazi cha Obote (walioshuhudia) utawala wake watakuambia kwamba wao ni kizazi cha 'nationalist' kwa maana maana walikuwa wakisoma kila pembe ya nchi na kwamba wanao marafiki kila kona pasipo suala ya ukabila kuweka mbele.
Nitakuja suala la Iddi Amini, naye singependa historia imu-hukumu vibaya. Tatizo la huyo bwana ni kwamba licha ya kuwa na mipango mizuri, hakuwa na fedha za kutekeleza maana wafadhili walimpa kisogo. Mfano mzuri ni kuwa master plan ya jiji la Kampala ilichorwa kipindi chake, na leo hii miaka kadhaa kupita kuna barabara imejengwa inaitwa 'northern bypass', architect wake ni Idd Amin! Lakini bado vile vile imechukuwa miaka 10 kuijenga (5-7kms) na gharama zake mara kumi ya ilivyopangwa. Ninatamani angalau barabara hiyo ingepewa jina lake maadam bado haijafunguliwa rasmi.
Kuhusu suala la Wa-baganda kumiminika barabarani baada ya Amini kuchukua madaraka, ni kwamba walidhani kwamba angelikuwa ni kibaraka wa kabila moja yaani 'Baganda'. Ukweli ni kwamba alianza kwa kufanya hivyo na mifano ni mingi, kwanza, alifanikisha kuurejesha mwili wa mfalme wa Buganda kutoka Uingereza. Hiyo ilimpa 'credit' kubwa sana. Pili, alipokwenda Canada kwenye mkutano, Iddi Amini akiwa si m-baganda, na kutokana na elimu yake kuwa sio kubwa ya kuweza kujieleza kwa ufasaha kwa lugha ya kiingereza, badala yake alizungumza 'ki-baganda'. Baada ya hapo ikawa kama kumkaribisha twiga kwenye kibanda ili apunge mvua, mwisho wake ni kukuondoa mwenye kibanda. Yaliyo mtokea Amini, ndio yanayomtokea Museverini sasa, maana naye aliingizwa madarakani kwa 'backing' ya wa-baganda wakidhani kwamba atabaki kuwa ni kibaraka wao. La hasha! mambo hayajaenda hivyo. Lakini tofauti kubwa kati ya Obote, Amini na Museverini, hakuna mtu zaidi ya Obote ambaye alijaribu kutaka kujenga misingi ya utaifa. Sasa hivi kinachotekea ni kuigawa Uganda kutokana na makabila. Na hii ni kuanzia na kuwa na waziri karibu kila kabila, na kila kabila kuwa na wilaya yake, kila kabila kuwa mfalme wao hata yale makabila ambayo hayajawahi kuwa na mfalme yanashauriwa yafanya hivyo, . Pia, ushawishi wa vikabila vidogo kujitoa kuwa chini ya himaya kubwa kama ya wa-baganda ambapo kihistoria imekuwa hivyo.
Ninaweza kuandika mengi lakini la msingi, aliyelewa madaraka ni nani kati ya hao watatu Obote, Amini na Museverini? Kumbuka Museverini ameomba 'ngwe' nyingine tena ya uraisi.
Tuendelee kubadilishana mawazo.
Mnyalu