Subscribe:

Sunday, July 31, 2011

Mgao Wa Umeme, Wataalamu Wasikilizwe; Asema Mbatia

Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia, akizungumza  na makada wa chama hicho wa mkoa wa Dar es Salaam mapema mchana wa leo katika ukumbi wa TRIZ Motel,Mbezi, jijini Dar es Salaam, kuhusu hali ya kisiasa nchini na changamoto za kiuchumi.Mbatia alisema kuwa suala la umeme linachukuliwa kisiasa na wataalamu hawapewi nafasi ya kupanga na kuamua nini kifanyike kumaliza mgao wa umeme.Akizungumzia juu ya kiti cha Spika na 'kashikashi' zinazotokea bungeni, Mbatia aliseama kuwa Spika Makinda anayumbishwa na Chama chake cha CCM, Kwani yeye binafsi haoneshi kuwa ana maamuzi na kubaki kusikiliza maelekezo kutoka kwa vigogo wa CCM.
Makada wa chama waliohudhuria mkutano huo.Picha zote na Victor Makinda
Reactions::

Kamati Maalumu Ya Wanafunzi Wa Chuo Cha Ustawi Wa Jamii. Taarifa Kwa Vyombo Vya Habari

Msemaji wa Kamati Maalumu ya Wanafunzi wa Chuo cha Ustawi wa Jamii, Boniface Benezeth, akisoma taarifa kwa waandishi wa habari (hawapo pichani), leo mchana jijini Dar es Salaam, kuhusu mgomo wa wanafunzi wa chuo hicho uliofanyika hivi karibuni. Picha na Victor Makinda
KAMATI MAALUMU YA WANAFUNZI WA TAASISI YA USTAWI WA JAMII
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Ndugu Wanahabari,
JULAI 21, 2011, Taasisi ya Ustawi wa Jamii (ISW) ilisitisha masomo (kufunga chuo) kwa muda usiojulikana kutokana na kile kinachotajwa kuwa ni mgomo usio halali wa wahadhiri. Hali hii ya kufunga chuo (kusitisha masomo) imekuwa na madhara makubwa kwa wanafunzi (wanachuo) ikiwa ni pamoja na wengi kukosa malazi na hata wengine kushindwa kujikimu kimaisha huku wengine muda wao wa ruhusa kazini ukimalizika.
Kutokana na hali hiyo, baada ya tangazo la kusitisha masomo kutolewa na Kaimu Mkuu wa Taasisi, Mlwande Madihi mbele ya Mkutano Mkuu wa Wanafunzi ikiwa yapata saa 11:15 jioni, wanafunzi wote wa Taasisi ya Ustawi wa Jamii katika Mkutano huo wakiongozwa na Rais wa Serikali ya Wanafunzi (ISWOSO) walikubaliana na kuunda Kamati Maalumu ya  Dharura kwenda Dodoma kuwasilisha kilio cha wanafunzi kwa Serikali na hasa ikizingatiwa kuwa kutokana na vikao vya Bunge la 10 kuendelea, wakiamini kuwa viongozi hao wa Serikali (Mawaziri na Manaibu Waziri) watapatikana kirahisi hukohuko.
JULAI 24, 2011 (Jumapili), Kamati ilifika Dodoma na ikiongozwa na Kaimu Mwenyekiti Chrisant Mutatina; Makamu Mwenyekiti Mariam Saad na Katibu Kitamogwa Safari. Ikiwa Dodoma, ilikutana na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa na kisha ikakutana na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Lucy Nkya.
Siku iliyofuata Kamati hiyo ikiwa na wajumbe 10 ilikaribishwa katika Kikao cha Bunge na soma zaidi http://www.kwanzajamii.com
Reactions::

JK Aongoza Kikao Cha Kamati Kuu Ya CCM

Mwenyekiti wa CCM Rais Dr.Jakaya Mrisho Kikwete akiongoza kikao cha Kamati kuu ya Halmashauri kuu ya CCM mjini Dodoma leo asubuhi.Wengine katika picha kutoka kushoto ni wajumbe wa kamati hiyo Rais mstaafu awamu ya pili Mzee Ali Hassan Mwinyi,Rais Wa Serikali ya mapinduzi ya Zanzibar Dr.Ali Mohamed Shein, Rais Mstaafu wa Zanzibar Amani Abeid Karume.Wengine katika picha ni katibu mkuu wa CCM Wilson Mkama na makamu wa CCM bara Pius Msekwa

Katibu Mkuu wa CCM Taifa Willson Mkama,akisoma utaratibu wakati wa kikao cha Kamati Kuu ya CCM Taifa kilichofanyika leo,katika ukumbi wa CCM Makao Makuu Dodoma,(wa pili kulia) Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais wa Tanzania Dk Jakaya Kikwete,makamo wa Mwenyekiti wa CCM Zanzibar,Dk Amaan Abeid Karume,Rais wa Zanzibar na Mjumbe wa kamatiu Kuu ya CCM Dk Ali Mohamed Shein,wakisikiliza kwa makini,taarifa zilizotolewa katika kikao hicho.(31/07/2011)
Reactions::

Soko Kuu Lateketea Kampala

Wachuuzi kama elfu kumi katika soko kuu la Owino mjini Kampala, wamepoteza mali zao zilizoteketea kwenye moto uliotokea Jumapili alfajiri.
Hii ni mara ya pili moto kutokea hapo katika kipindi cha miaka miwili.
Polisi walisema wanachunguza. BBC
Reactions::

Rais Wa Zanzibar Asoma Risala Ya Mwezi Mtukufu Wa Ramadhani

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk Ali Mohamed Shein, akisoma risala ya kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhan na kuwatakia wananchi kheri kati mfungo huo kwasalama,pia kuwataka wajitahidi katika kufanya ibada kwa wingi na kuzidisha imani katika jamii.
Picha na Ramadhan Othman,IKULU.
Reactions::

Wanafunzi Darasa La Saba Wauza Kuni Kulipia Gharama Za Mitihani


Wanafunzi wa shule ya msingi Manda wakitoka kusaka kuni porini kwa ajili ya kuuza na kupata shilingi 600 ya mchango wa mitihani
WAZAZI wa wanafunzi wa darasa la saba ambao wanangoja mtihani wa Taifa wa kuhitimu elimu ya msingi katika shule ya msingi Manda wamekuwa na hofu ya watoto wao kufeli mtihani wa Taifa wa darasa la saba kutokana na uongozi wa shule hiyo kuwafukuza wanafunzi wasio kulipa mchango wa shilingi 600 michango ya mitihani na wakati mwingine kuwatuma kutafuta kuni za walimu.



Wakizungumza na hivi karibuni na mwandishi wa habari hizi, wazazi hao ambao ni JOhn Haule na Hosea Nkera kwa pamoja walisema kuwa tabia ya uongozi wa shule hiyo kuwafukuza madarasani wanafunzi hao wa darasa la saba wasio lipa mchango wa shilingi 600 iwapo haitakemewa upo uwezekano wa watoto wao kufanya vibaya mtihani huo.
Walisema kuwa wakati shule nyingine za msingi kwa wakati huu wa kuelekea katika mtihani wa Taifa wa darasa la saba walimu wamekuwa wakikesha wakiwakumbusha watoto yale waliyofundishwa ili kujiweka vizuri kwa mitihani hiyo ila shule hiyo imekuwa ikitumia muda mwingi kuwatumikisha wanafunzi hao katika kazi zawalimu za kutafuta kuni porini na kufanya kazi nyingine za walimu huku baadhi yao wakifukuzwa kufuata michango kwa wazazi.
Alisema Haule kuwa baadhi ya wazazi katika kata hiyo ya Manda wana hali mbaya kiuchumi na hawana fedha za kuwalipia wanafunzi hao kiasi hicho cha shilingi 600 kwa ajili ya kufanya mtihani wa kujipima na kupelekea idadi kubwa ya wanafunzi hao wa darasa la saba kujiingiza katika shughuli za uvuvi katika ziwa nyasa kutafuta samaki wa kuuza ili kupata fedha hizo na wale wasio na uwezo wamekuwa wakilazimika kushinda mitaani .
Hivyo alimwomba afisa elimu wa wilaya hiyo ya Ludewa na serikali kupiga marufuku walimu kuwatumikisha ama kuwafukuza wanafunzi hao wa darasa la saba wasio na michango kwani kufanya hivyo ni kupelekea matokeo ya ufaulu kwa wanafunzi hao kuwa mabaya zaidi.
Nkwera aliwataka walimu wa shule hiyo kutowasumbua wanafunzi hao kwa michango na kuwa iwapo shule kuna mradi unaendeshwa basi uwe kati ya wazazi na wananchi wote wanaozunguka shule husika badala ya kuwalenga wanafunzi pekee ambao hawana uwezo wa kupata fedha hizo.
Alisema kwa upande wake ana watoto wawili ambao wanasoma shule hiyo darasa la saba na kuwa uwezo wa kuwalipia shilingi 1200 kwa ajili ya mtihani kwa sasa hana .
Mmoja kati ya walimu wa shule hiyo ambaye hakupenda kutaja jina lake kwa madai kuwa si msemaji wa shule hiyo alisema kuwa utaratibu huo wa michango uliamuliuwa katika kikao cha pamoja kati ya wazazi na viongozi wote wa kata hiyo ya manda na kuwa fedha hizo ni kwa ajili ya kuchangia gharama za usimamizi wa mitihani na chakula kwa walimu wanaofika kusimamia mitihani ya kujipima ngazi ya kata.
Diwani wa kata ya Manda Efrida Kizota alisema kuwa hakuna kikao ambacho kilikaa na kuamua wanafunzi kuchangia gharama za mkitihani na kuwa uongozi wa shule hiyo unafaya makosa kuwafukuza wanafunzi kwa kufuata michango hiyo isiyo na baraka kutoka kwa wazazi na wananchi.
Afisa elimu wa shule za msingi wilaya ya Ludewa Robart Hyella alisema kuwa amepokea malalamiko ya wazazi juu ya walimu wa shule hiyo kufukuza wanafunzi kwa ajili ya kukosa michango na kuwa amemwagiza mratibu wa elimu kata kufuatilia suala hilo. Francisgodwinblog





Reactions::

Denmark Na Korea Kusini Zaisaidia Tanzania 592 Bilion

Waziri wa Fedha Mustafa Mkulo (kushoto ) akibadilishana hati ya msaada wa shilingi bilioni 318 na Balozi wa Korea Kusini Young hoon Kim (kulia) jana jijini Dar es salaam kwa ajili ya ujenzi wa njia ya usambazaji umeme kutoka Iringa, Shinyanga , ujenzi wa Majengo ya Chuo Kikuu cha Tiba cha Muhimbili na maandalizi ya vitambulisho vya kitaifa.
Picha na Tiganya Vincent, MAELEZO- Dar es salaam



Reactions::

Alfajiri Ya Leo Tunaruka Kurudi Nyumbani Kwenye Ndege Wetu!

Mimi, makamanda wangu na mama yao. Kama kila kitu kitakwenda sawa, basi,  saa tano usiku wa leo Jumapili tutakuwa  Dar. Ama kweli, nyumbani ni nyumbani. Nimewakumbuka sana ndugu, jamaa na marafiki. Nimewakumbuka ndege wa nyumbani pia. Iringa ninakoishi, kila alfajiri  huamshwa na sauti za kuvutia za ndege wa porini. Mara moja moja bundi hulia pia. Pichani ni siku Mrisho Mpoto  aliponitembelea nyumbani kwangu Iringa. Kamanda wangu hakuchelewa kutoa burudani ya muziki kwa kupiga gitaa lake. Naam, nimefurahia sana vekesheni yangu ya Ulaya. Ahsanteni sana wote ambao, kwa namna moja ama nyingine, mmenikarimu ' Mwenyekiti' wenu nilipokuwa hapa Sweden. Panapo majaliwa nitarudi tena, sijui lini. Kila la kheir kwenu nyote!
Reactions::

Saturday, July 30, 2011

Bilioni 30 Zatengwa Na Serikali Kwa Ajili Ya Mradi Wa Maji Wilayani Masasi

Serikali imetenga shilingi bilioni 31 kwa ajili ya Mradi wa maji wa Mbwinji wilayani Masasi utakaohudumia pia wilaya ya Nachingwea.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete amewaeleza wananchi wa Masasi hayo katika uwanja wa sabasaba Julai 28 katika muendelezo wa ziara yake mkoani humo.
Mradi huo mkubwa ambao chanzo chake cha maji ni mto Nanguu unagharamiwa na serikali unatarajiwa kukamilika katikati ya mwaka 2012.
Rais yuko mkoani Mtwara kuwashukuru wananchi kwa kumchagua yeye na Chama chake Cha Mapinduzi kuliongoza tena Taifa la Tanzania na pia kukagua utekelezaji wa ahadi za uchaguzi.

Tatizo la maji ni kero kubwa kwa wananchi wa wilaya nyingi mkoani humu ikiwemo Masasi na Nanyumbu.

Mara baada ya kuwasili wilayani Masasi Rais amepokea taarifa ya wilaya za Masasi na Nanyumbu na kusikitishwa na taarifa za kuongezeka idadi ya watoto wanaopata mimba katika shule za msingi na sekondari

“Sijafurahishwa na mimba za watoto wa kike wa shule za msingi na sekondari si jambo jema”. Rais amesisitiza na kuwataka wanaume waache watoto wasome.
“Wanaume ndiyo chanzo cha tatizo hili, ni jambo la ovyo na watoto wa kike shughulikeni na jambo moja tu”. Rais amewaasa.

Rais ameshatembelea wilaya za Mtwara Mjini, Vijijini, Tandahimba, Newala, Masasi na Nanyumbu ambapo amemalizia ziara yake ya kikazi mkoani Mtwara na anatarajia kurejea jijini Dar es Salaam tarehe 29 Julai, 2011.

Mwisho.

Imetolewa na Premi Kibanga,
Mwandishi wa Habari wa Rais Msaidizi,
Mkoani Mtwara.
29 Julai, 2011
Reactions::

Bajeti Ya Marekani Imekwama

Mjadala kati ya wanasiasa, kuhusu bajeti, na jinsi ya kuzidisha kiwango cha mkopo wa serikali ya Marekani ungali umekwama.     Ufumbuzi unatakiwa ufikiwe kabla ya Jumaane, ambapo Wizara ya Fedha itaanza kupungukiwa na fedha za kulipia matumizi ya serikali.
Ijumaa usiku, baraza la wawakilishi, ambalo wabunge wake wengi ni kutoka chama cha Republican, lilipitisha mswada kuzidisha kiwango cha mkopo na kupunguza matumizi ya serikali, lakini mswada huo ulikataliwa na baraza la Senate, lenye wajumbe wengi wa chama cha Democrat.
Hali ya uhasama na mashindano imetanda Washington huku Jumaane inakaribia.
Wanasiasa bado wanavutana wakati wanahitaji kupatana ili kuepuka wasi-wasi na pengine matafaruku katika uchumi wa Marekani, ikiwa muafaka haukufikiwa kabla ya tarehe ya mwisho, yaani tarehe mbili Agosti.

Mswada uliopendekezwa na wabunge wa chama cha upinzani cha Republican Ijumaa, katika baraza la wawakilishi, ulizimwa katika baraza la Senate, ambako wajumbe wa chama cha Democrat sasa wanashindana na upinzani, na wanajaribu kusukuma mbele pendekezo lao wenyewe.

Lakini mswada huo piya, uliopendekezwa na kiranja wa chama cha Democrat, Harry Reid, unafanyiwa kazi ili ukubalike kwa wengi.
Vikao kati ya wanasiasa vitaendelea weekendi nzima na huenda makubaliano yakafikiwa dakika ya mwisho, na hatimaye kuwatuliza raia na masoko.BBC
Reactions::

Naibu Spika Atunikiwa CPA London

Tuzo yenyewe kama inavyoonekana.

Spika wa Bunge Mhe. Anne Makinda (Mb) akiwa katika picha ya Pamoja na Naibu Spika wa Bunge la Uingerza Mhe. Nigel Evance (Mb) (Mwenye tai) pamoja na Mwenyekiti Mpya wa CPA Mhe Sir Alan Heselhurst (Mb) mara baada ya kumalizika rasmi kwa mkutano wa 57 wa CPA ambao ulifanyika London Uingereza kwa kukutanisha Maspika, Maseneta na Wabunge zaidi ya 700 kutoka nchi 52 za Jumuiya ya Madola kujadili maswala mbalimbali yahusuyo uendeshaji wa Mabunge katika mabunge wanachama wa Jumuiya hiyo . Wengine katika picha ni Ujumbe wa Tanzania ulioambatana na Mhe. Spika katika Mkutano huo na Katibu Mkuu wa CP Dkt William Shija ( Nyuma ya Spika)

Mwakilishi wa Chama cha Wabunge wanawake wa Jumuiya ya Madola Afrika (CPA) katika Mkutano Mkuu wa 57 wa CPA Dunia Mhe. Beatrice Shelukindo akipokea tuzo kwa niaba ya Naibu Spika Mhe. Job Ndugai kutoka kwa mwenyekiti wa CPA anayemaliza mda wake Mhe. Mohamed Shafie Apdal kutoka Malaysia ambayo Mhe Ndugai amezawadiwa kwa kuitumikia kamati tendaji ya CPA kwa mda wa Miaka mitatu. Mhe. ndugai amekuwa mjumbe wa Kamati kuu tendaji ya CPA tangu mwaka 2008 ambapo mda wake umekwisha mwaka huu. Mkutano Mkuu wa CPA umemalizika Jana jijini London Uingereza. Picha na Owen Mwandumbya wa Bunge

Spika wa Bunge Mhe. Anne Makinda akimwaga rasmi Naibu Spika wa Bunge la Uingerza Mhe. Nigel Evance mara baada ya kumalizika rasmi kwa mkutano wa 57 wa CPA ambao ulifanyika London Uingereza kwa kukutanisha Maspika, Maseneta na Wabunge zaidi ya 700 kutoka nchi 52 za Jumuiya ya Madola kujadili maswala mbalimbali yahusuyo uendeshaji wa Mabunge katika mabunge wanachama wa Jumuiya hiyo . Picha na Owen Mwandumbya wa Bunge
Reactions::

Wamependeza! Nadir Na Malin

Osterfarnebo, Sweden. Jana jioni.
Reactions::

Ya Madini Na Nishati Ni Kioja Kingine! ( Makala, Raia Mwema)

 Na Maggid Mjengwa,

PTOLEMY, mwanafalsafa wa Kiyunani alipata kuandika: ”Ex Africa simper aliquid novi". Maana yake: "Kila kukicha kitazuka kioja kingine Afrika."
Naandika makala haya nikiwa nchini Sweden. Katika kufuatilia yanayoandikwa na kusemwa na wanahabari wa Sweden kutuhusu sisi, basi, nimekutana na kashfa ambayo kimsingi ni kioja chenye kutuhusu.
Hapa Sweden kuna Shirika la Misaada limeishinikiza Serikali ya Sweden kuacha kufadhili kwa kuyapa mitaji ya kuwekeza makampuni yenye kukwepa kodi kama ilivyo kwa kampuni ya Pan African Energy.
Kampuni hii Pan African Energy iliyosajiliwa kwenye visiwa viwili; Mauritius na Jersey, inavuna gesi ya Songosongo nchini Tanzania; huku ikiwa imeingia mkataba wa miaka 25 na TANESCO kupitia Shirika la Taifa la Maendeleo ya Petroli , TPDC. Ni mkataba wenye kuifanya kampuni hiyo kutokulipa kodi ya faida ya mapato wanayopata kutokana na mauzo ya umeme unaotokana na gesi asilia wanayovuna Songo Songo.
Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Action Aid, iliyotolewa mwezi Mei mwaka huu, tangu Pan African Energy waanze kuvuna gesi asilia kule Songo Songo mwaka 2004, kampuni hiyo imevuna faida ya zaidi ya dola za Kimarekani milioni 60. Nusu ya faida hiyo ilipatikana mwaka 2009 na kampuni hiyo ilitarajiwa kuongeza uzalishaji. Hivyo, kuvuna zaidi gesi yetu asilia ya Songosongo.
Mpaka kufikia sasa, Pan African Energy imefanikiwa kukwepa kodi inayokadiriwa kufikia dola za Kimarekani milioni 10. Hiki ni kiasi cha fedha kinachotosha kusomesha watoto wa Kitanzania 175,000 ( Laki moja na sabini na tano elfu) kwa mwaka kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Action Aid.
Kwa kifupi tu, ripoti hii inadhihirisha namna ufisadi uliotamalaki unavyochangia kutuacha Watanzania tukiwa katika hali ya giza linalotokana na mgawo wa umeme. Unatuacha tukiwa katika hali ya uzalishaji duni kutokana na uhaba wa nishati ya umeme. Ufisadi umetuletea giza na umasikini.
Kampuni hii ya Pan African Energy inanufaika na mkataba wa kifisadi usiotanguliza maslahi ya Taifa. Taarifa hii niliweka mtandaoni majuma mawili yaliyopita na hakika wengi wameshiriki kuitolea maoni yao.
Ni jambo la faraja na kutia moyo kuwa hata waheshimiwa wabunge, bila kujali itikadi zao za vyama, wameanza kuamka na kuwa wakali kutetea rasilimali zetu. Na hakika, huu ni wakati wa waheshimimiwa wabunge wetu kumweka kikaangoni Waziri wa Nishati na Madini Mh. William Ngeleja ili atoe maelezo ya kina juu ya kashfa hii ya Pan African Energy. Na Waziri Ngeleja atwambie ni hatua gani zitachukuliwa na lini kwa wote waliochangia kutufikisha kwenye kashfa hii, na hivyo basi kutufikisha katika giza hili tunalolishuhudia sasa kwa kukosa nishati hii muhimu kwa maana ya umeme.
Naamini kuwa nchi yetu ni nchi tajiri sana, lakini wananchi wake wengi wamo katika lindi la umasikini unaotokana na ufisadi wa wachache tuliowapa dhamana za uongozi.
Haiyumkini mtu mwenye akili zake na anayeipenda nchi yake akakubali kuingia mkataba wa miaka 25, kwa maana ya robo karne, na kampuni ya kigeni kuruhusu wageni hao wavune gesi yetu asilia iliyo kwenye visima vyetu kule Songo Songo.
Na kioja katika mkataba huo ni mgeni mwekezaji anayevuna gesi yetu tunakubali asitozwe kodi kwa faida anayopata kwa kutuuzia umeme unaotokana na gesi ya kwetu wenyewe! Kwa mwanadamu, ni heri uwe mwendawazimu kuliko kuwa limbukeni. Watanzania tumefanywa kuwa malimbukeni.
Na majuzi hapa tumemsikia Mbunge wa Kilindi (CCM), Beatrice Shellukindo, akimtuhumu Bungeni Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo, kwa kutumia Shiolingi bilioni moja kwa ajili ya kutoa rushwa kwa watu mbalimbali ili bajeti ya wizara hiyo iweze kupitishwa na Bunge. Nacho ni kioja kingine kwa wizara ya serikali kutumia fedha kuwahonga wawakilishi wa wananchi ili bajeti ipite, na wawakilishi hao wakapokea hongo hiyo.
Ni jambo jema kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda kufikia busara ya kuondoa bungeni hotuba ya makadirio ya matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini. Na itakaporudi tena bungeni, ni wakati wa wabunge wetu kusimammia maslahi ya umma na kuibana Wizara kufafanua baadhi ya mikataba yenye kashfa kama huu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli, TANESCO na kampuni ya Pan African Energy.
Na kauli ifuatayo ya Mbunge wa Nzega, Mheshimiwa Hamisi Kingwangwalah inatia matumaini kuwa bado tuna wabunge walio tayari kupambana kutetea maslahi ya umma.
Mbunge Kingwangwalah aliyasema haya bungeni:
"Nataka nianze kwa kusema siungi mkono hoja ya kupitishwa kwa bajeti hii na nawaomba wabunge wenzangu msipitishe bajeti hii kwa sababu tupo gizani". Mbali na tatizo la umeme, alitaja sababu nyingine za kutaka bajeti hiyo isipitishwe kuwa ni mikataba mibovu ya sekta ya madini na nishati ambayo imesababisha rasilimali za nchi kuibwa na wageni huku Watanzania walio wengi wakiendelea kuogelea kwenye umasikini.
Mbunge Kingwangwala anasema: "Waliosababisha hayo wanajulikana lakini hawachukuliwi hatua. Wengine wapo hapa bungeni na wengine wako serikalini. Hii ni mikataba kandamizi. Watu hao wapo kwenye 'system' (mfumo wa Serikali). Nchi inauzwa, wachache wanashibisha matumbo yao. Watu hawa wamelifikisha taifa kwenye mazingira haya ya kifisadi kwa sababu ya kutumia nafasi zao kujinufaisha na kuweka kando maslahi ya umma wa Watanzania...Hawa watu kama hawafikirii kwa matumbo wanafikiria kwa kutumia 'spinal cord' (uti wa mgongo) badala ya ubongo."

Mbunge huyo akaongeza kusema; “ Watendaji walioliingiza taifa kwenye mikataba hiyo mibovu wanapokwenda kuisaini wanajali kile watakachopata ili kufanikisha malengo yao binafsi kama vile kujenga majumba ya kifahari. Wanaruhusu ardhi ya Watanzania kuuzwa nao wanafaidi kwa kwenda kujenga Mbezi Beach (Dar es Salaam),"


Akaongeza kusema: “Miongoni mwa mikataba ya kifisadi ni kati ya
Pan African na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuhusiana na uzalishaji na usafirishaji wa gesi asilia.” Mwisho wa kumnukuu.
Ndio, kuna baadhi ya viongozi wetu wameigeuza nchi yetu kuwa Banana Republic. Katika Banana Republic, wanasiasa wachache hutumia siasa kufanya biashara na uchumi wa nchi. Wako tayari kuuza rasilimali za nchi kwa faida yao.
Watanzania tuna lazima ya kukataa kugeuzwa malimbukeni na kuruhusu nchi yetu kuwa Banana Republic’- Jamhuri ya Migomba. Nahitimisha.
Reactions::

Tanzania: Ni Vigumu Kutimiza Matumaini Ya Vijana Katika Dunia Ya Utandawazi


MAELEZO YA PICHA:
Mwakilishi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Ombeni Sefue akizungumza wakati wa Mkutano wa Kilele wa Vijana uliofanyika Makao Makuu ya  Umoja wa Mataifa ukiwashirikisha vijana kutoka mataifa mbalimbali, mawaziri wanaohusika na masuala ya Vijana na Taasisi za kijamii. Akizungumza  mbele ya wajumbe wa mkutano huo, Balozi Sefue amesema Utandawazi na matumizi ya vyombo vya habari vya kijamii ( Social Media) siyo tu kumewafanya vijana kuwa katika kijiji kimoja lakini pia  vijana wamekuwa na matumaini na mwamko mkubwa  kisiasa, kijamii, kiuchumi na kitamaduni na kwamba kasi waliyonayo vijana hivi sasa inashindana na kasi ya serikali nyingi katika kuwatimizia mahitaji yao zikiwamo ajira.

Na Mwandishi Maalum
New York

Imeelezwa  kwamba  baadhi ya nchi zitashindwa kutekeleza kwa kasi matarajio na matumaini makubwa waliyonayo vijana.
Matarajio  na matumaini hayo ni yale yanayoletwa na  utandawazi na matumizi mkubwa ya vyombo vya habari vya kijamii.
Tahadhari  hiyo imetolewa na  Mwakilishi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Ombeni Sefue.Alikuwa akizungumza katika  Mkutano wa  kilele wa   Vijana uliofanyika Makao Makuu  ya Umoja wa Mataifa.
Amesema  utandawazi  ambao unaendeshwa na  teknolojia unawafanya vijana  kuwa  katika  kijiji kimoja cha kimataifa. Na kuwajengea ufahamu mkubwa wa wapi walipo au wapi wanatakiwa kwenda.
Balozi Sefue akaeleza  , Utandawazi  huo umewajengea  vijana matumaini makubwa ya kisiasa, kiuchumi , kiutamaduni na kijamii.“ Lakini, baadhi ya matarajio hayo  hayawezi kutekelezwa na serikali nyingi  kupitia  raslimali zilizonazo au sera zilizopo na kwa kasi wanayoitaka vijana”.
 “ kwa maneno mengine, ingawa Utandawazi unawapa  matarajio kwa vijana wetu, lakini siku zote utandawazi huohuo hautoi nyenzo sahihi za kuwapatia uwezo na fursa vijana ya kutimiza ndoto zao”.akasisitiza Balozi Sefue
Akatahadharisha  kuwa  kutotimizwa kwa ndoto hizo za vijana, kunaweza kusababisha madhara makubwa. Madhara ambayo  yanaweza kuvuka mipaka  ya nchi.
Kwa hiyo akasema, ni muhimu  kuunga mkono juhudi za serikali za kitaifa na kikanda, za kuujenga uutandawazi wa haki utakao wawezesha vijana siyo tu kuwa na matumaini bali pia kuwa  na fursa ya kumiliki mali.
Kuhusu matumizi ya vyombo vya habari  vya kijamii ambayo vijana wengi wanajitanabaisha navyo, Balozi  Sefue amewaeleza wajumbe wa mkutano huo kwamba, ingawa vyombo hivyo ni nyezo  muhimu katika kuleta mabadiliko chanya. Kwa bahati mbaya vyombo hivyo kama havitatumia ipasavyho vinaweza pia kuleta matokeo mabaya.
Mwakilishi huyo wa Tanzania katika UM, akabainisha kuwa serikali yake inaamini kwamba vijana siyo tu  viongozi wa kesho, kwani wanaweza kuwa viongozi wa leo na kutoa mchango mkubwa wa kulijenga taifa lao kwa kushirikiana na  wazee wao.
Akasema kwa kutambua umuhimu wa ushiriki wa vijana katika ujenzi wa nchi yao, ndio maana serikali ya Tanzania  imepitisha  sera zinazo wawezesha vijana wa kike na kiume kupata nafasi za uongozi   katika vyombo vya utoaji wa maamuzi  likiwamo Bunge.
Mkutano huo ambao  ulifunguliwa na Katibu Mkuu wa  Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, uliwashirikisha mawaziri wanaohusika na masuala ya vijana kutoka nchi wanachama wa UM. Pamoja na mambo mengine ulijadili changamoto mbalimbali zinazowakabili vijana duniani kote na namna ya kuzitafutia ufumbuzi.
Mkutano huo pia ulihudhuriwa na mamia ya vijana kutoka sehemu mbalimbali duniani. Pamoja na wawakilishi kutoka taasisi zisizo za kiserikali. Na   ulitoa na maazimio mbalimbali yakiwamo ya kubuni mbinu mbadala za kushughulikia matatizo ya vijana  zikiwamo ajira.



Reactions::

Hamkulijua Hili; ' Mwenyekiti' Wenu Anapenda Ukoko!



Jana nilialikwa mlo wa mchana mji wa Gavle hapa Sweden. Nilikaribishwa wali kwa choroko ama chooko kama wanavyoita wengine. Basi, mwenyeji wangu akanipakulia wali. Nikamwomba anikwangulie na ukoko.

Naam, wali ni ukoko ati. Na kuna matandu na ukoko. Mie napenda ukoko. Na raha ya ukoko uule chunguni ukiwa umeuloweka kwa mchuzi wa maharage. Na kama ukoko umelowana haswa, basi, unaukwangua kwa vidole. Ndio, mla ni mla ukoko, mla wali amebwia wa chuya! Haya basi, unayefikiria siku moja kumkaribisha ' mwenyekiti' wako wali na maharage, basi, usisahau na ukoko wake!
Reactions::

Friday, July 29, 2011

JK Akikagua.....



1. Rais Dr.Jakaya Mrisho Kikwete akikagua ubanguaji unaofanywa na wakulima wadogo katika kijiji cha Kitama,Wilayani Tandahimba wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Mtwara.
2. Rais dr.Jakaya Mrisho Kikwete akikagua korosho iliyosindikwa kwa mashine katika kiwanda cha Rift Valey Foods, wilayani Tandahimba. ( Picha: Freddy Maro)
Reactions::

JK Ziarani Newala, Tandahimba Na Nanyumbu





1. Rais Dr.Jakaya Mrisho Kikwete akiweka jiwe la msingi katika ghala jipya za mazao wilayani Tandahimba.
2. Rais Dr.Jakaya Mrisho Kikwete akikagua chanzo cha Maji ya mradi wa Makonde Water Supply katika bonde la Kitangari wilayani, Newala, mkoani Mtwara wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Mtwara.
3. Rais Dr.Jakaya Mrisho kikwete na  kaimu mganga mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu Dr.Zulkarnain Ikaji wakifunua kitambaa katika jiwe la msingi kuashiria kuzindua rasmi Zahanati ya Sengenya, iliyopo wilayani Nanyumbu, mkoani Mtwara jana.
4. Kaimu Mganga mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu Dr.Zulkarnain Ikaji akimwonesha Rais Dr.Jakaya Mrisho Kikwete gari la kubebea wagonjwa aina ya bajaj litakalotumika katika Zahanati ya Sengenya wilayani Nanyumbu jana (Picha; Freddy Maro)
Reactions::

Dr Salim Ahamed Salim Azindua Maadhimisho Miaka 50 YaKumbukumbu Ya Mwalimu Nyerere

Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere ,Kivukoni na Waziri Mkuu Mstaafu Dkt Salim Ahmed Salimu akizindua maadhimisho ya miaka 50 ya Chuo hicho jana(leo) jijini dare s salaam.Chuo hicho kianzishwa tarehe 29 Julai mwaka 1961.Wageni wengine ni pamoja na Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Sinde Warioba
Wanajumuiya wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere , Kivukoni wakimsikiliza kwa makini hotuba ya uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 50 ya Chuo hicho iliyotolewa jana(leo) jijini Dar es salaam na Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo hicho na Waziri Mkuu Mstaafu Dkt Salim Ahmed Salim(hayupo pichani).Picha Zote na Tiganya Vincent- MAELEZO- Dar es salaam.
Mkuu wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere,Kivukoni Dkt John Magotti akitoa hotuba ya ukaribisho leo jijini Dar es salaam wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 50 ya uanzishwaji wa Chuo hicho.
Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Sinde Warioba akitoa mada juu ya mchango wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere katika maendeleo ya ya Taifa leo jijini Dar es salaam wakati wa uzindua maadhimisho ya miaka 50 ya Chuo hicho.Chuo hicho kianzishwa tarehe 29 Julai mwaka 1961

Mawaziri Wakuu Wastaafu Jaji Joseph Sinde Warioba(kushoto) na Dkt Salim Ahmed Salimu(kulia) wakibadilishana mawazo leo jijini Dar e salaam wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 50 ya uanzishwaji wa Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Kivukoni

Reactions::

CCM Kilimanjaro Wawajulia Hali Majeruhi Wa Ajali

Magari yaliyopata ajali.
Katibu wa CCM mkoa wa kilimanjaro,Steven Kazidi,akimpa pole Bi.Esimend Parimina ambaye amelazwa katika Hospital ya Rufaa ya KCMC baada ya kujeruhiwa jicho lake la kulia katika ajali ya basi la Lim Safari iliyotokea juzi jioni eneo la kibosho road nje  kidogo ya Manispa ya Moshi,watu 11 walipoteza maisha yao na wengine 26 kujeruhiwa vibaya.Picha na Mdau Bashir Nkromo. 

CHAMA cha Mapinduzi(CCM) mkoa wa Kilimanjaro,kimetoa pole kwa majeruhi wa ajali ya Basi iliyotokea juzi jioni katika bara bara ya kibosho road nje kidogo yaManispaa ya Moshi.



Katika ajali hiyo iliyohusisha basi la Lim Safari lenye namba za usajili T489BJR na roli la mizigo aina ya Bitisubishi Fuso lenye namba za usajili T884BFJ likiendeshwa na dereva wake Sifael Kaaya,watu 11 walifariki papo hapo wakiwamo madereva wote wa magari hayo mawili. Wote waliofariki ukiondoa madereva hao,ni vibarua waliokuwa wakirejea makwao
huko machame wilaya ya Hai wakitoka kuvuna kahawa katika shamba la kahawa laKilimanjaro Plantretion Ltd ambalo lipo eneo la Kibosho wilaya ya Moshi Vijijini.


Mashuda wa ajli hiyo walisema dereva wa basi hilo,alikuwa amelewa na hakuweza kusikia kilio cha abiria wake waliomtaka apunguze mwendo.
Akitoa pole jana katika Hosiptal ya rufaa ya KCMC baada ya kutembelea majeruhi
wa ajli hiyo,katibu wa CCm mkoa wa Kilimanjaro,Steven Kazidi,alisema ajali hiyoinatoa funzo kwa mamlaka husika kuwajibika katika kusimamia sheria za usalama barabarani.


Katibu huyo alisema kuwa,aajli nyingi zinatokea kutokana na uzembe wa madereva na kutaka jitihada zifanywe na vyombo husika kutoa adhabu kali kwa madereva wanaosababisha ajali.Alisema Chama cha Mapindizi CCM kimeguswa na ajali hiyo na katika kuonesha kwavitendo,CCM ilitoa msaada wa sh,600,000 na kati ya hizo sh,300,000 zilitolewa na Umoja wa Vijana wa CCM(UVCCM) Manispaa ya moshi .
Msaada huo aliutoa kupitia kwa Mkurugenzi wa Idara ya uuguzi katika Hospital hiyo ya KCMC Redempta Mamseri aliyepokea kwa niaba ya Mkurugenzi wa Hospital hiyo,Moshi Ntabae.
Kazidi ambaye alitembelea Idara ya upasuaji katika hospital hiyo na kuzungumza na baadhi ya majeruhi ,alifuatana na katibu wake msaidizi,Habas Mwijuki, Kamanda ya UVCCM Manispaa ya Moshi Agrrey Marealle na Katibu wa CCM Manispaa ya
Moshi,Amos Shimba.
Kwa upande wake kamanda wa UVCCM Manispaa ya Moshi,Agrrey Marealle ,alitioa wito kwa serikali kuona umhimu wa ajali za barabarani kuongezwa katika orodha ya majanga ya kitaifa pamoja na kuweka sheria kali za kudhibiti uzembe kwamadereva.
Aidha Marealle alishauri serikali kuboresha elimu ya madereva kwa kutoa elimu juu ya sheria za usalama barabarani,kudhibiti mianya ya rushwa ikiwamo biashara ya leseni bandia na pia kuwa na utaratibu wa madereva kurudia majaribia ya udereva(driving test) mara kwa mara .
Alishauri pia kuweka mkazo katika kuwadhibiti madereva wanaoendesha vyombo vya moto huku wakiwa wamelewa,kupunguza safari za usiku pamoja na kutoa muda wa kupumzika kwa madereva wa mabasi ya abiria na magari ya mizigo bila hivyo taifa litaendelea kupoteza nguvu kazi hasa vijana.
"Bila hivyo tutaendelea kupoteza watu hususani vijana ambao ndiyo raslimali kuu ya nchi,kampeni hii inahitaji ushirikiano kati ya polisi na serikali,vyama vya siasa,vyombo vya habari,madhehebu ya dini na jamii kwa ujumla"alisema Marealle.



Reactions::

Ludacris Atinga Viwanja Vya Jangwani Sekondari

Mwanamuziki kutoka nchini Marekani Ludacriss, akiwasalimu wanafunzi wa shule ya sekondari ya Jangwani leo jioni wakati mwanamuziki huyo alipokwenda kutoa zawadi kwa mshindi wa shindano la nyimbo za kuhamasiaha mapambano dhidi ya Malaria, kampeni inayojulikana kwa jina la Zinduka, Malaria haikubaliki.
Wanafunzi wa Jangwani sekondari
Ludacriss akitoa zawadi kwa washindi wa shindano la nyimbo za kuhamasiha kampeni dhidi ya Malaria, ZINDUKA MALARIA HAIKUBALIKI, leo jioni katika viwanja vya shule ya sekondari Jangwani.  Wanafunzi wa shule ya sekondari Azania ndio walioshinda na hapo wakipokea zawadi ya toka kwa Ludacris.
Ludacris  (katikati) akiwa na wasanii wa  Bongo Fleva wa hapa nyumbani, leo jioni katika viwanja vya shule ya sekondari ya Jangwan. (Picha na mpigapicha wa mjengwablog)



Reactions::

Jeshi La Polisi Tanzania: Taarifa Kwa Vyombo Vya Habari


Mnamo tarehe 22/7/2011 Inspekta Jenerali wa Polisi Said Alli Mwema alitoa wito kwa wananchi wote kupitia vyombo vya habari kuwa, katika utekelezaji wa kampeni ya kutii sheria bila kushurutishwa wale wote wanaomiliki silaha isivyohalali wazisalimishe kwa hiari na zinazomilikiwa kihalali zihakikiwe upya. Na zoezi hili ni kwa muda wa miezi mitatu (3) kuanzia tarehe 1 Agosti hadi Octoba 31, 2011. Katika kipindi hicho hakutakuwa na hatua zozote za kisheria zitakazochukuliwa dhidi ya mtu atakayesalimisha/kuhakiki silaha kwa hiari yake.


3. Tunawashukuru wananchi ambao wameanza kuitikia wito huo kwa kuanza kusalimisha silaha zao kwa hiari. Pamoja na hayo, inaonekana bado kuna makundi ya watu/watu ambao bado wanaendelea kumiliki na kufanyia uhalifu silaha wanazozimiliki isivyo halali.
4. Mfano wa matukio hayo ni kama ifuatavyo, mnamo tarehe 28/7/2011 majira ya saa 7 usiku katika Mkoa wa Kagera wilaya ya Biharamuro, wananchi wema walitoa taarifa polisi kuwa, kuna majambazi yapatayo 6 katika eneo la pori lililopo kati bwanga na Bihalamuro wamejipanga kuteka magari ya abiria/ mizigo yanayopita katika eneo hilo, baada ya polisi kupata taarifa hizo, walienda katika eneo hilo na ghafla majambazi hayo yalianza kuwafyatulia risasi. Katika kurushiana risasi Polisi walifanikiwa kuyaua majambazi yote sita (6) na kufanikiwa kupata silaha 2 aina ya SMG na risasi 180.


5. Aidha, katika tukio jingine la kusikitisha mnamo tarehe 27/7/2011 majira ya usiku huko katika kijiji cha Genkuru Tarime Rorya askari Polisi No. F. 4268 D/C Pendo aliuawa kwa kupigwa risasi shingoni na jambazi aitwae Bhoke Mohere waliyekuwa wameenda kumkamata nyumbani kwake kwa kosa la unyanganyi wa kutumia silaha na kumiliki silaha isivyo halali. Baada ya mauaji hayo jambazi hilo lilifanikiwa kutoroka.


6. Hali hii, inadhihirisha wazi ni jinsi gani askari polisi wanafanya kazi katika mazingira hatarishi, pamoja na kwamba wanakuwa wanatekeleza majukumu yao kwa kufuata matakwa ya sheria, lakini kuna mahali wanakutana na mazingira ya watu wabaya wanaokaidi kutii sheria, hali inayopelekea askari wenyewe kuuawa ama kujeruhiwa. Na hii ina maana kwamba nguvu anayoitumia mhalifu katika kupambana na askari ndiyo inayomlazimu askari Polisi kuona atumie nguvu kiasi gani ili aweze kumdhibiti mhalifu huyo.
8. Wito wangu kwa jamii, wakati zoezi hili linaendelea nawaomba wananchi wote waendelee kutoa taarifa za watu wanaowafahamu ambao wanamiliki silaha isivyohalali ili kusaidia kuwabaini endapo watakaidi agizo la kusalimisha silaha hizo kwa hiyari.


Imeandaliwa na
Advera Senso- ASP
Msemaji Mkuu wa Jeshi la Polisi
Tanzania.



Reactions::

Awamu Ya JK Kwenye Televisheni Ya Sweden; Tafsiri Yangu

Ndugu zangu,


Katika miezi ya karibuni, nchi yetu Tanzania, katika hali isiyo ya kawaidia kwenye media ya nchi za Magharibi, mara kadhaa imezungumzwa katika sura chanya kwenye vyombo vya habari vya nchi ya Sweden ikiwamo televisheni yao ya taifa.



Huko nyuma nimepata kukaa Sweden kwa miaka kumi na miwili; 1992-2004 sura ya Tanzania iliyokuwa ikionyeshwa kwenye media ni kuwa ni moja ya nchi masikini Afrika na inayotegemea misaada ikiwamo misaada kutoka nchi ya Sweden tangu miaka ya 1970. Ni kama mtoto anayenyonyeshwa kila anapolia njaa.



Lakini, katika mfululizo wa vipindi vya Televisheni “ Det Nya Afrika"-ikiwa na maana ya ' Afrika Mpya' vilivyoonyeshwa mapema mwaka huu kwenye televisheni ya taifa ya Sweden, mwandishi Erica Bjorstrom alitembelea Tanzania mara kadhaa. Mwandishi huyu anaitaja Tanzania kuwa mfano mzuri wa nchi iliyoanza kusimama na kuinuka kiuchumi. Unaweza kuona moja ya vipindi hivi kwa lugha ya Kisweden ukitembelea;
Tanzania: Välståndet växer - Rapport | SVT Play


Kwa mujibu wa mwandishi huyu, uchumi wa Tanzania ni moja ya uchumi unaokua kwa kasi kubwa barani Afrika. Kwamba uchumi wa Tanzania unakua na hali za maisha ya watu zimeanza kuwa bora. Inasemwa , kutokana na kukua huko kwa uchumi na kuongezeka kwa mapato yanayotokana na kodi,Tanzania imeanza hata kufikiria kutoa malipo ya pensheni kwa wasio katika mfumo rasmi wa ajira kwa mfano wakulima.



Mwandishi huyu anatoa sababu mbili zinazopelekea Tanzania kuinuka kiuchumi; Mosi,Tanzania imetoka kwenye mfumo wa chama kimoja na kuingia kwenye vyama vingi, pili, kuwepo kwa mfumo wa soko huria na kuruhusu watu kuendesha shughuli za viwanda na biashara.



Mwandishi huyo wa televisheni anatoa mfano wa moja ya viwanda vya kampuni ya Azam; ni kiwanda cha kusindindika matunda. Kwamba kinachangia kuinua uchumi wa nchi kwa kutoa ajira, kununua mazao ya wakulima na hata kuchangia uchumi wa Sweden kwa vile kampuni ya vifaa vya viwandani ya Sweden, ABB inauza vifaa na vipuri vya viwandani kwa kampuni hiyo ya Azam.



Katika moja ya vipindi hivyo vya televishen mwandishi huyu Erica Bjostrom anaongea na gavana wa Benki Kuu, Benno Ndulu . Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania anatoa picha ya Tanzania iliyojizatiti kuinua uchumi wake kwa kujenga uchumi unaotegemea sekta nyingi.



Pia mwandishi huyo anamhoji Balozi wa Sweden nchini Tanzania , Bw. Lennarth Hjalmaker ambaye anakubali kuwa uchumi wa Tanzania unakua na kuwa Sweden, kama nchi, imeanza kujipanga kubadili aina ya misaada inayotoa kwa Tanzania. Sweden sasa inafikiria zaidi katika kuisaidia Tanzania katika maeneo ya biashara na viwanda.



Hayo ni machache tu katika mengi mazuri ambayo Tanzania na hususan utawala wa Awamu ya Nne wa Rais Jakaya Kikwete umepambwa nayo na mmoja wa nchi wafadhili wakubwa wa Tanzania tangu tupate uhuru, Sweden. Ni sifa ambazo nilikutana nazo kutoka kwa baadhi ya raia wa Sweden tangu siku ya kwanza nilipotua Sweden yapata majuma sita yaliyopita.



Ni mtazamo huo chanya wa kimaendeleo ya kiuchumi kwa Tanzania kutoka kwa watu wa kawaida wa Sweden ndio ulionifanya nipekue mtandaoni kuona ni nini hasa kilichoripotiwa na vyombo vya habari vya Sweden juu ya Tanzania.



Tafsiri yangu;


Vyombo vya habari vina nguvu kubwa ya kuathiri mitazamo ya watu . Kazi ile ya mwandishi Erica Bjostrom imechangia kuifanya Tanzania, machoni mwa watu wa Sweden kuwa ni nchi yenye kuleta matumaini ya kuwa mfano wa taifa la Kiafrika linalopiga hatua kutoka hali ya ukale na kuingia kwenye kuwa taifa la kisasa zaidi. Mara nyingi, hilo la mwisho ndilo lenye kuiletea nchi na watu wake heshima zaidi.


Na taifa la kisasa ni lile lenye kuheshimu misingi ya utawala bora ikiwamo kuamini katika demokrasia ya mazungumzo na si ya virungu . Taifa la kisasa ni taifa lenye kuruhusu uwazi zaidi na si kuruhusu usiri hata kwenye masuala ya msingi yenye maslahi kwa umma. Mfano hapa ni uwepo wa mikataba ya siri. Ni mikataba yenye kuhusu rasilimali za wananchi kufanywa kuwa jambo la siri.



Ndio, taifa la kisasa lazima liachane na ubaguzi wa kisiasa. Tanzania, tangu awamu ya kwanza imeendesha siasa za kibaguzi ikiwa na maana kuwabagua wale wote wenye fikra tofauti na kuwapiga mihuri ya wasaliti, wapinzani na majina mengineyo. Na tunayoyavuna leo ikiwamo ufisadi uliotamalaki unaolitafuna taifa ni matunda ya ubaguzi wa kisiasa ambao mbegu zake zimepandwa miaka 50 iliyopita.



Tumekuwa ni watu wa hovyo hovyo. Watu tusiotanguliza maslahi ya taifa bali ya chama, na hakika si ya chama, bali maslahi binafsi na ya kimakundi. Ni watu wa hovyo hovyo tunaotanguliza udini na ukabila badala ya utaifa.


Kwenye makala ya ’ Neno la Leo’ niliyoandika usiku wa kuamkia leo nimesimulia kisa cha Mfalme Ihsani kwenye nchi ya bahari ya giza.


Ndio, popote panapotokea maendeleo makubwa na ya haraka, basi, hutokea pia mabadiliko yenye kuyakwaza na kuyavunja maendeleo hayo. Ni mambo yenye kusababishwa na ubinafsi, chuki, husuda, fitina, wivu na siku hizi kuna neno mizengwe pia. Yote hayo ndio haswa ’ Magamba’ tuliyo nayo Watanzania. Hayo si magamba ya chama cha siasa tu. Ni magamba ya kitaifa.Kuyavua hayo sharti ukokwe moto ili kuipasha moto kwanza miili yetu!



Tufanye nini?



Umefika wakati sasa kwa Chama na Serikali iliyopo madarakani ijenge ujasiri wa kukubali kuwa Tanzania ni muhimu zaidi kuliko Chama cha siasa au watu mmoja mmoja. Kiandae mazingira yasiyokuwa na mizengwe ya kuandaa Katiba itakayowatoa Watanzania walio wengi kwenye umasikini wa kudhalilisha unaotokana na ubaguzi wa kisiasa. Maana, nchi yetu ni nchi tajiri sana ila watu wake ndio masikini kutokana na maovu ya wachache tuliowapa dhamana ya kutuongoza.



Ona Finland . Haka ni ka- nchi kadogo sana katika dunia hii. Lakini ni moja ya nchi tajiri sana na ambazo Tanzania kama nchi, viongozi wake hupita huko kutembeza bakuli la ’ Saidia Masikini!’.



Ndugu zangu,


Ka- nchi ka Finland kale uchumi wake ulianza kwa kutegemea miti ya mbao nyepesi. Hawana miti ya mpingo wala misonobali. Lakini kwa vile hawaendekezi ubaguzi wa kisiasa na kuwa wanatanguliza maslahi ya nchi yao, wameweza kujenga miundo mbinu imara ikiwamo ya hata akilini kwa maana ya elimu.


Sisi Watanzania tuna miti ya mipingo, dhahabu, almasi, gesi asilia, uranium, makaa ya mawe, Tanzanite,mito, maziwa, bahari, mbuga za wanyama na mengine mengi. Lakini bado tunaona hata fahari kujitambulisha kuwa; ” Sisi ni nchi masikini bwana!”


Na tuna viongozi wanaosimama hadharani na kutamka kuwa ni vizuri tukabaki na mfumo wa chama kimoja. Vyama vingi vitatuletea vita!”

Na kiongozi mwingine katika kuendekeza ubaguzi wake wa kisiasa anatamka hadharani; ” Ukitaka biashara yako ikuendee vizuri njoo CCM!”

Ni fikra kama hizi za ukale ndizo zitakazomfanya mwandishi Erica Bjostrom na wengine wa dunia hii kurudi tena Tanzania na kuripoti habari ya nchi ya Tanzania iliyoonyesha dalili za kusimama na kukimbia, kuwa sasa inaangamia tena kwa machafuko ya kisiasa na watu kuuana. Na sababu kubwa itakuwa ni ubaguzi wa kisiasa wenye kujenga misingi ya hila katika chaguzi.



Naam, wahenga walinena; ngoma ikivuma sana hupasuka. Ndio maana ya kusema; Pavumapo palile, si kazi kudamirika!



Maggid



Sweden,


Ijumaa, Julai 29, 2011
Reactions::